…Watuhumiwa wakiwa ndani ya mahakama
Mwanasheria kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Johanes Kalungula akizungumzia tukio hilo.
VIGOGO watano wa Kampuni ya mawasiliano ya Six Telecoms Limited wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na makosa ya kuhujumu uchumi ukiwemo utakatishaji fedha wa zaidi ya Sh. Bilioni 8.
Vigogo hao ni Mhandisi na Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, Hafidhi Shamte, mfanyabiashara na Mkurugenzi, Peter Noni, Mwanasheria, Mhadhiri na Mkurugenzi wa hiyo kampuni, Ringo Tenga, Mkuu wa Fedha, Noel Chacha na Kampuni yenyewe ya Six Telecoms Limited.
Watuhumiwa hao wamesomewa makosa yao na Wakili wa Serikali, Jehovaness Zacharia,mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Victoria Nongwa.
Akizungumza mahakamani hapo, Wakili Zacharias alidai kati ya Januari 1, 2014 na Januari 14, 2016 jijini Dar es Salaam washtakiwa, walitoza malipo ya simu za kimataifa kwa kiwango cha Dola 0.25 kwa dakika kwa lengo la kujipatia faida.
Watuhumiwa hao wanadaiwa kati ya Januari Mosi, 2014 na Januari 14, 2016 kwa udanganyifu na kwa nia ya kuepuka malipo, walishindwa kulipa kiasi cha Dola za Marekani 3,282,741.12 kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kama mapato.
Washtakiwa hao wanadaiwa kati ya Januari Mosi 2014 na Januari 14, 2016 walishindwa kulipa ada za udhibiti za Dola 466,010.07 kwa TCRA.
Kampuni ya Six Telecoms Limited inadaiwa kati ya JanuarI 2014 na Januari 14, 216 ilitumia Dola 3,282,741.12 wakati ikijua fedha hizo ni zao la makosa ya udanganyifu yanayotokana na mashtaka yaliyotangulia.
Baada ya washtakiwa hao kusomewa mashtaka hayo hawakuruhusiwa kuongea chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka katika kesi hiyo hadi Mahakama Kuu ambapo wakili wa utetezi aliiomba mahakama iondoe hati ya mashtaka kwa sababu alidai kuna baadhi ya makosa ya mapungufu ya kisheria.
Hakimu Nongwa ameahirisha kesi hiyo hadi Novemba 24 mwaka huu.









Post a Comment