Benki ya Dunia (WB) itashirikiana na Serikali ya Tanzania katika kukabiliana na athari za mafuriko zinazosababishwa na mvua kubwa zinazonyesha kila mwaka katika Jiji la Dar es Salaam hasa eneo la Jangwani.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango wakati akizungumza na ujumbe wa Benki ya Dunia katika mikutano ya kipupwe inayoendelea mjini Washington DC.
Dkt. Mpango amesema Benki ya Dunia imekubali kusaidia kukabiliana na mafuriko katika bonde la mto Msimbazi hasa katika eneo la kutoka Magomeni Mapipa kwenda Faya na tayari Benki hiyo imeanza zoezi la kutafiti eneo la Jangwani ili kuweza kuangalia namna nzuri ya kugharamia uboreshaji wa mifereji katika bonde la mto Msimbazi.
“Tumewaeleza changamoto ambayo imekuwa inajirudia kila mara na kusababisha upotevu wa maisha ya watu, kusababisha kufungwa kwa barabara, watu kushindwa kwenda kazini na wanafunzi kushindwa kwenda shule, hivyo wameonesha nia ya kumaliza kero hii kwa wananchi,” alisema Dkt. Mpango.
Amesema kuwa baada ya timu ya Benki ya Dunia kumaliza kufanya kazi yao kwa kushirikiana na Manispaa ya jiji la Dar es Salaam, Serikali inaamini njia ya kudumu itapatikana na kuondokana na tatizo hilo.






Post a Comment